Thursday, February 2, 2012

Maiti ya jambazi Arusha yazua 'kasheshe'


Ndugu wasusa mwili mochari, wachukuliwa na Mchungaji 

NDUGU wa jambazi sugu aliyeuawa na polisi Januari 13
mwaka huu, Bw. Pokea Kayaa (45), maarufu 'Steven Kaunda', wamesusa kuchukua maiti yake katika Hospitali ya Mount Meru, mjini Arusha.
Kutokana na hali hiyo, Mchungaji wa Kanisa la Tumaini Assemblies of God, wilayani Arumeru, Amani Silanga, akiwa na baadhi ya watu waliomfahamu Bw. Kaaya, walilazimika kwenda hospitali kuchukua mwili huo na kuusafirisha jijijini kwake Nkoanrua.

Akiongoza ibada ya mazishi kijijini hapo, Mchungaji Silanga alisema kitendo kilichofanywa na ndugu wa Bw. Kaaya si cha kiungwana na hakileti tija katika jamii.
Ninachoamini ni kwamba, ndugu wa Bw. Kaaya na jamaa zake wa karibu, wameshindwa kujitokeza na kwenda kuchukua mwili wake hospitali wakihofia kukamatwa na kuhojiwa polisi jinsi walivyomfahamu marehemu,¡± alisema.
Aliongeza kuwa, ndugu hao hawakupaswa kuogopa kwani kifo cha marehemu kimetokana na matendo aliyokuwa akiyafanya duniani hivyo upo umuhimu wa kila mmoja kuangalia mwenendo wake, kujiepusha na maovu ili kuishi maisha mazuri katika jamii.
Alisema kifo cha Bw. Kaaya kiwe changamoto kwa jamii kuacha vitendo vya uhalifu ambayo matunda yake ndiyo hayo na kutoa pole kwa Jeshi la Polisi na familia ya marehemu.
Aliongeza kuwa, yeye binafsi hakuwa na woga wa kwenda kuchukua mwili wa marehemu Mochari kwa hofu ya kuhusishwa na matendo aliyokuwa akiyafanya Bw. Kaaya.
Bw. Kaaya alikuwa akitafutwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kujihusisha katika matukio mbalimbali ya uhalifu likiwemo la mauaji ya askari wa upelelezi mwenye namba F 2218, Konstebo Kijanda Mwandu na kumjeruhi Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Arusha Bw. Faustine Mafwele.
Jambazi huyo aliuawa saa 12:45 asubuhi akiwa kwa mganga wa kienyeji wakati akipatiwa matibabu yaliyotokana na jeraha la risasi.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi mkoani Arusha, Thobias Andengenye, alisema polisi walipata taarifa za kuwepo Bw. Kaaya katika Kitongoji cha Lengine, Kijiji cha Orarashi, wilayani hapa Januari 13 mwaka huu.
Alisema Bw. Kaaya alikuwa boma la mganga wa kienyeji Bi. Anna Roshilari, ambapo polisi baada ya kufika eneo hilo, walizunguka boma hiyo kwa lengo la kumkamata.
Askari walilizunguka boma usiku, ilipofika saa 12:45 asubuhi, ghafla Bw. Kaaya alitoka nje na kuanza kutimua mbio ndipo askari walipoanza kumfukuza umbali wa kilomita mbili.
Huyu jambazi alisimama na kumvamia askari mwenye namba E 9912 Konstebo Wito, na kumng¡¯ata vidole vya mkononi ili aachie bunduki aliyokuwa nayo,¡± alisema.
Kamanda Andengenye aliongeza kuwa, kutokana na maumivu makali, askari huyo alilazimika kuachia silaha yake, lakini wakati Bw. Kaaya akikaribia kuichukua, askari wengine wakafika haraka na kumpiga risasi na kufa papo hapo.
Alisema Jeshi la Polisi bado linawashikilia watoto wa marehemu
Alex Parumina (13) na Daines Massawe (9), ambao walikamatwa siku ya tukio la mauaji ya polisi, Januari 3 mwaka huu, katika eneo la Shangarai na Bi. Rehema Ally, ambaye alikamatwa na silaha akiwa ameificha chooni.
Januari 6 mwaka huu, polisi kwa kushirikiana na wananchi wa eneo la Moshono, Mtaa wa Letera, walifanikiwa kupata silaha ya jambazi huyo alizoyotumia kuua na kujeruhi.
Bunduki hiyo ni Sub Machine Gun (SMG) yenye namba za usajili 1016188011 ikiwa na risasi 20, magazine mbili na Shotgun aina ya Model yenye namba za usajili 88-12GA ikiwa na risasi nne.

Na Richard Konga, Arusha

1 comment:

  1. Jambazi ni mtu hatari sana, akikuwahi tu huna lako, kwa hiyo tuwe polisi jamii

    ReplyDelete


Labels